NEW DELHI, India
WAZIRI Mkuu wa Uingereza David Cameron amekataa kurejesha taji la malkia lililotengenezwa kwa dhahabu, na kuzawadiwa Malkia Victoria wa Uingereza miaka ya 1800. Malkia Victoria alitawala Uingereza
kuanzia Juni 30, 1837 hadi Januari 22, 1901, ambapo alizawadiwa taji hilo lililopewa jina la Koh-i-noor, kwa maana ya mlima wenye mwanga. Cameron aliuzwa swali hilo alipokuwa akihojiwa kwenye televisheni, kama Uingereza inaweza kurejesha taji hilo la dhahabu, ambapo alitoa jibu la hapana. Kwa mujibu wa taarifa zilizo tolewa na wasomi wa Kihindu, taji hilo liligunduliwa miaka 700 iliyopita. Taarifa zilisema kuwa taji hilo lilichukuliwa na kampuni ya British East India baada ya mji wa Punjab kutekwa na majeshi ya Uingereza mwaka 1849. Na baadaye taji hilo lilitolewa zawadi kwa Malkia Victoria. Cameron alisema kurejesha taji hilo kutahatarisha vitu vingine vya kiutamaduni vilivyowekwa kwenye makumbusho za Uingereza. Alitoa mfano kuwa Ugiriki imekuwa ikidai kurejeshewa vitu vya kumbukumbu, vilivyochukuliwa nchini humo miaka 200 iliyopita.








