NA GRAYSON YOHANESS, TSJ
KOCHA wa timu ya taifa ya vijana chini ya miaka 20, 'Ngorongoro Heroes', Rodrigo Stockler amewaita wachezaji watatu kuziba nafasi ya mshambuliaji nyota wa kikosi hicho, Thomas Ulimwengu kitakachovaana
na Ivory Coast Agosti 8, Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam. Ngorongoro Heroes ilichapwa bao 1-0 na Ivory Coast katika mchezo wa kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20. Ili timu hiyo isonge mbele inahitaji kupata ushindi wa zaidi ya mabao 2-0. Akizungumza Dar es Salam, Stockler aliwataja wachezaji hao ni ni Abdallah Bunu wa JKT Ruvu, Mbwana Samatta na Kelvin Charles kutoka Simba ambapo mmoja kati yao ataziba pengo la mshambuliaji huyo anayetoka kituo cha Tanzania Soccer Academy (TSA) kilichopo chini ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF). Alisema kuwa ameamua kuchukuwa uamuzi huo ili kuweka tahadhari kwa kuwa Ulimwengu akishinda majaribio ya kucheza soka ya kulipwa nchini Sweden atakosa mchezo huo muhimu. Stockler alisema vijana wake wapo kwenye mazoezi makali kujiandaa na mchezo huo aliodai utakuwa vita kali kwa Ngorongoro Heroes ambayo inasaka tiketi ya kucheza fainali hizo zilizopangwa kupigwa mwakani nchini Libya. Alisema anatarajia kupata upinzani mkali kutoka kwa wapinzani wao aliodai kuwa timu yao ni nzuri na inaundwa na wachezaji sita wanaocheza soka ya kulipwa. Stockler alisema Ngorongoro Heroes inatarajiwa kucheza michezo ya kirafiki dhidi ya timu ya ligi kuu Villa Squad iliyopangwa kuchezwa keshokutwa kabla ya kuzivaa timu za vijana za Azam FC na Simba kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.








